Rebeka: Bibi-Arusi Aliyeamini Ujumbe wa Mjumbe

Siku moja, Abrahamu alimwita mtumishi wake mwaminifu, Eliezeri. Alikuwa na kazi muhimu sana ya kumpa afanye. Alipaswa kutoka katika nchi ya Kanaani na kwenda kumtafutia mwanaye Isaka mke. Abrahamu alijua jinsi kazi hiyo ilivyokuwa muhimu, lakini alikuwa na imani kubwa kwa mtumishi wake, Eliezeri. Alijua kwamba yeye ndiye mtu sahihi kwa ajili ya kazi hiyo!
Eliezeri alikusanya ngamia kumi wa Abrahamu, pamoja na dhahabu na vitu vingine vyote alivyohitaji kwa safari hiyo. Hakuwa na wazo lolote la jinsi angemtafutia Isaka mke, lakini alimtegemea Mungu na akaendelea mbele na safari yake.
Muda si mrefu, Eliezeri alijikuta karibu na Mji wa Nahori, huko Mesopotamia. Ilimbidi afanye uamuzi. Je, atembee huku na kule akitafuta msichana mzuri zaidi katika mji huo, au aachie jambo hilo mikononi mwa Mungu kabisa, na Yeye Mwenyewe aamue Isaka aoe nani?
Mtumishi mkuu Eliezeri alifanya uamuzi sahihi: aliamua kumwachia Mungu jambo hilo. Mara moja, alikuwa kando ya kisima cha maji nje ya mji, akaanza kuomba.
"Tazama, ninasimama hapa kando ya kisima cha maji; na binti za watu wa mji watatoka kuteka maji; na itakuwa hivi, kwamba yule msichana nitakayemwambia, Tafadhali shusha mtungi wako nipate kunywa; naye ataniambia, Kunywa, nami nitawanywesha na ngamia zako pia; huyo ndiye utakayekuwa umemteua kwa mtumishi wako Isaka..."
Eliezeri aliomba kwamba msichana sahihi angemruhusu anywe maji katika mtungi wake, na si hivyo tu, bali pia angetoa maji kwa ngamia wake.
Wakati huo huo, Eliezeri alipokuwa bado anaomba, msichana mrembo mmoja alitoka kuelekea kisimani. Baada ya kujaza mtungi wake, Eliezeri alikimbia kumlaki.
"Tafadhali niruhusu ninywe maji kidogo katika mtungi wako," Eliezeri alimwomba.
"Kunywa, Bwana wangu," Rebeka mrembo alijibu.
Eliezeri huenda alikuwa akitabasamu alipokuwa akinywa kutoka mtungi wa Rebeka. Je, huyu ndiye? Je, Bwana alikuwa anajibu maombi yake haraka namna hiyo? Alijua kwamba kama yeye ndiye aliyekusudiwa kwa Isaka, angejitolea kunywesha ngamia wake pia.
Kisha akasema maneno sahihi, "Nitawatekea maji na ngamia wako pia, mpaka wamalize kunywa."
Eliezeri alisimama pale akimtazama Rebeka mrembo akiwanywesha ngamia mpaka wasiweze kunywa tena. Mungu alikuwa amejibu maombi yake, Alikuwa amemtuma Rebeka awe mke wa Isaka!
Eliezeri alishawishika kabisa kwamba yeye ndiye, hivyo akamwambia Rebeka sababu halisi iliyomleta huko. Alimwelezea kila kitu kuhusu Abrahamu, na mwanaye, Isaka.
Rebeka aliamini kila kitu Eliezeri alichomwambia, akamwamini amtunze katika safari ya kurudi kumkuta mume wake mpya, Isaka.
Ilikuwa lazima iwe safari ya kusisimua kwa Rebeka kijana. Eliezeri huenda alimwelezea yote kuhusu Isaka na jinsi alivyokuwa mtu bora, na jinsi angekuwa mume mzuri. Rebeka alizidi kusisimka zaidi na zaidi mpaka siku ile hatimaye ilipofika alipomwona kwa mara ya kwanza!
Isaka alikuwa shambani wakati macho yao yalipokutana. Ulikuwa ni upendo wa mtazamo wa kwanza, na yote hayo yalitokana na mtumishi mwaminifu wa Abrahamu, Eliezeri, na imani ya Rebeka kwake.
Hii ni hadithi nzuri sana inayowakilisha sisi leo. Kama vile Abrahamu alivyokuwa akimtafutia Isaka mke, ndivyo Mungu anavyomtafutia Bibi-arusi kwa ajili ya Mwanaye, Yesu. Kama vile Abrahamu alivyomtuma Eliezeri, Mungu pia alimtuma mjumbe mwema na mwaminifu, Ndugu Branham, kutafuta Bibi-arusi kwa ajili ya Mwanaye.
Kazi yetu ni kama ile ya Rebeka. Tunapaswa kumsikiliza mjumbe, kuamini anachotuambia, na kujiandaa kukutana na Yule anayetuambia habari zake: Yesu!
Unaweza kusoma habari za Rebeka katika Mwanzo, Sura ya 24